Saa za Kazi

Fahamu kuhusu saa za kazi za Tanzania, sheria inasemaje kuhusu saa za kazi za ziada, malipo ya saa za kazi za zaidi, overtime n.k

Ni sheria zipi zinazosimamia saa za kazi kwa sekta binafsi Tanzania?
 Kipengele kidogo B cha Sheria ya Ajira na Mahusiano ya Kazi ya mwaka 2004 kinaelezea kuhusu saa za kazi Tanzania.

Je ni kipi kiwango cha juu cha muda wa kufanya kazi kwa siku kilichoelezwa na sheria?
Kiwango cha juu kabisa cha saa za kazi ambacho mfanyakazi anaruhusiwa na sheria kufanya kazi ni saa 45 kwa juma ambayo ni sawa na saa tisa (9) kwa siku. Saa tisa hizi ni tofauti na saa moja litolewalo kwa ajili ya chakula cha mchana. Mapumziko ya chakula cha mchana hutolewa baada ya saa tano mfululizo za kufanya kazi. Mapumziko haya hua hayalipwi na ni muda wa mfanyakazi pekee, mfanyakazi anaweza kusoma kitabu, kufanya manunuzi, kufanya mazoezi n.k kwa sababu hawalipwi kwa muda ule wa mapumziko. Muda wa ziada zaidi ya saa 45 kwa juma lazima ulipwe kama saa za ziada. Pia sheria inakataza mfanyakazi kufanya kazi zaidi ya saa 12 kwa siku.
Mfanyakazi anaruhusiwa kufanya kazi siku sita za wiki na kupumzika siku ya saba.


Je kuna kikomo cha muda wa saa za ziada ambacho mfanyakazi anaweza kufanya kazi?Kama jibu ni NDIO, je naweza kujadili na mwajiri wangu kuongeza muda huo?
Mwajiri haruhusiwi kumtaka au kumruhusu mfanyakazi kufanya kazi kwa saa za ziada kama hawana makubaliano. Hata panapokua na makubaliano mwajiri na mfanyakazi hawaruhusiwi kuzidisha wastani wa muda wa saa za ziada kama ilivyoelezwa katika sheria za kazi, ambazo ni saa 50. Kwa hiyo sheria imeweka kikomo cha saa za ziada ambacho mfanyakazi anaweza kufanya kazi. Kipengele cha 19 (3) kinakataza mfanyakazi kufanya kazi zaidi ya saa za ziada zinazozidi 50 katika mzunguko wa wiki nne.


Je ninastahili kiwango gani cha malipo kwa kufanya kazi saa za ziada?
Mwajiri atatakiwa kumlipa mfanyakazi si chini ya moja na nusu ya mshahara wa mfanyakazi kwa muda wa saa za ziada uliotumika. Ikitokea saa za ziada zikatumika katika siku za mapumziko au za sikukuu basi mfanyakazi atalipwa kwa kiwango cha mara mbili zaidi ya malipo ya kawaida kwa kila saa alilofanya kazi.

Je malipo haya ni tofauti kama nitafanya kazi usiku?
Sheria inafafanua usiku kua ni kipindi kati ya saa mbili usiku na kabla ya saa kumi na mbili (12). Kama utafanya kazi muda wa usiku utastahili kulipwa angalau asilimia 5% ya mshahara wako kwa kila saa ulilofanya kazi usiku na kama ni saa za ziada basi 5% itakokotolewa katika kiwango cha saa za ziada. Hata hivyo, si kila mfanyakazi anaefanya kazi usiku anastahili 5% iliyoelezwa hapo juu, hii ni kwa wale tu ambao kwa kawaida hufanya kazi muda wa mchana lakini kwa sababu za dharura watahitajika kufanya kazi usiku. Watu kama walinzi, wauguzi wanaofanya kazi kwa zamu, wahudumu wa migahawa na hoteli wafanyao kazi kwa zamu hawastahili hii 5%.

Nina miaka 16/mjamzito/mgomjwa, je naweza kuendelea kufanya kazi za usiku?
Ni kinyume cha sheria kwa mwajiri kumruhusu mtu katika makundi yafuatayo kufanya kazi usiku;
•    Mtoto chini ya miaka 18
•    Mfanyakazi aliethibitishwa kua mgonjwa na hivyo kushindwa kufanya kazi za usiku
•    Mfanyakazi mjamzito mwenye miezi miwili kabla ya kujifungua
•    Mfanyakazi mjamzito mwenye miezi miwili au zaidi kabla ya kujifungua kama amethibitisha na daktari kushindwa kufanya kazi za usiku
•    Mwanamke kufanya kazi nyakati za usiku kwa kipindi cha miezi 2 baada ya siku ya kujifungua
•    Wazazi kufanya kazi za usiku baada ya kutoa vithibitisho kuthibitisha afya yao hairuhusu kufanya kazi za usiku au afya ya mtoto hairuhusu mama kufanya kazi za usiku.
Je kuna uwezekano wa kuingia makubaliano na mfanyakazi ili kuongeza muda wa kufanya kazi hadi saa 12 bila ya saa za ziada?
NDIO, lazima kuwe na makubaliano ya maandishi kati ya mfanyakazi na mwajiri ambao utaeleza wazi kua utahitajika kufanya kazi hadi saa 12 kwa siku kujumlisha muda wowote wa kula bila ya kupata malipo yoyote ya ziada. Hahivyo katika mfumo huu hutaruhusiwa kufanya kazi zaidi ya siku 5 za wiki, zaidi ya saa 45 kwa wiki na zaidi ya saa 10 za ziada kwa wiki. Makubaliano ya pamoja kati ya mwajiri na chama cha wafanyakazi yanaweza pia kuweka wastani wa saa za ziada na saa za kawaida katika kipindi fulani cha makubaliano. Kama ilivyo katika makubaliano ya maandishi, makubaliano ya pamoja hayatoruhusu mfanyakazi kufanya kazi zaidi ya wastani wa saa 40 kwa wiki zinazokokotolewa katika kipindi cha makubaliano, saa 10 za ziada kwa wiki na haitokubali kuzidi kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja.

Loading...